Je, Mbu Wanapendelea Kundi Fulani la Damu? Wanasayansi Wafafanua
Utafiti mwingine uliochapishwa mwaka 2021 kwenye jarida la kisayansi Nature Scientific Reports ulionyesha kuwa mbu wa kike hupendelea kundi la damu B. Hata hivyo, baada ya marekebisho, utafiti huo uliondolewa rasmi mwezi Juni 2022, baada ya watafiti kubaini kuwa kundi la damu O lina kiwango kikubwa cha usagaji wa damu mwilini.
Wanasayansi Wanasemaje?
Healthy Nation ilizungumza na Dkt. Eric Ochomo, mtaalamu wa wadudu na Naibu Mkurugenzi wa Kituo cha Utafiti wa Magonjwa ya Kuambukiza na Vimelea katika Kemri.
Majibu yake yalikuwa wazi — mbu hawajali kundi la damu la mtu.
Lakini kuna mengine zaidi.
Anasema mbu huvutiwa na binadamu kwa sababu ya mambo mengi ikiwemo harufu ya mwili — si lazima iwe harufu mbaya, bali ni mchanganyiko wa kemikali zinazotoka kwenye ngozi ya binadamu. Harufu hizi huchangiwa na lishe, jasho, na wakati mwingine vinasaba vya mtu (genetics).
Aidha, mbu huvutiwa na miili yenye joto zaidi. Dkt. Ochomo anaeleza kuwa ingawa joto la kawaida la mwili ni 37°C, linatofautiana kati ya 36.4°C hadi 37.2°C. Hii ndiyo sababu baadhi ya watu huhisi joto zaidi kuliko wengine, na mbu wanaweza kubaini ni nani ana joto zaidi.
Sababu nyingine ya kawaida ya mbu kuvutiwa kwako ni hewa ya kaboni dayoksaidi (CO₂). Anasema kuwa mbu huvutiwa sana na hewa tunayotoa tunapopumua. Usiku unapolala na kupumua, ni kama unaimba wimbo wa kuwakaribisha mbu.
Anabainisha kuwa ingawa tafiti kadhaa zimeonesha kundi la damu O linaweza kuvutia zaidi mbu, bado matokeo hayo si ya mwisho na mambo mengine yaliyotajwa hapo juu yana nafasi kubwa zaidi.
Profesa Jonathan Day, mtaalamu mstaafu wa Entomolojia ya Tiba kutoka Chuo Kikuu cha Florida, aliandika katika The Conversation kuwa kwa ujumla, mbu hutumia macho, sauti na uwezo wao wa kunusa kutambua chanzo cha damu. Anaeleza kuwa kwa kaboni dayoksaidi, licha ya kuwa magari pia hutoa hewa hiyo, mbu ni werevu kiasi cha kutambua ipi inatoka kwa binadamu na ipi ni ya chanzo kisicho na uhai.
"Michakato ya mwili kama kupumua na kusogea huzalisha harufu kama lactic acid, ammonia na asidi za mafuta ambazo huwasaidia mbu wa kike kunusa walipo watu," anaeleza.
Kuhusu harufu za mwili, anasema baadhi ya mbu huvutiwa na harufu ya miguu ya mtu, jambo ambalo huwasaidia kuhakikisha humwamshi mtu kutoka usingizini.
Basi, Tunazuiaje Mbu Wanaosababisha Malaria?
Kuna njia mbalimbali za kuzuia mbu. Wanasayansi wamefanya juhudi kubwa kuhakikisha kuwa kuna chanjo dhidi ya malaria. Mwaka 2021, Shirika la Afya Duniani (WHO) liliidhinisha chanjo ya kwanza kabisa dhidi ya malaria, ambayo tayari imeanza kutolewa kwa watoto nchini.
Njia nyingine za jadi za kujikinga na malaria ni pamoja na matumizi ya vyandarua vilivyowekwa dawa, vipulizia wadudu na dawa za kuua mbu.
Mwezi Desemba mwaka jana, Dkt. Ochomo na timu yake kutoka Kemri walizindua kifaa kipya cha kuzuia mbu kwa njia ya harufu. Kifaa hicho kinaning'inizwa ukutani kama fremu ya picha na hufanya kazi kama coil ya mbu, lakini hakitoi moshi na huchukua mwezi mzima kabla ya kuisha. Tofauti na njia nyingine zinazowazuia mbu, hii huwaua kabisa mbu wanaokaribia.
0 Comments